Saudi Arabia itaandaa mazungumzo ya kwanza ya ana kwa ana siku ya Jumamosi kati ya majeshi yanayopigana nchini Sudan, baada ya usitishaji mapigano mara kadhaa kutibuka.
Taarifa ya pamoja ya Marekani na Saudia imekaribisha kuanza kwa "majadiliano ya kabla ya mazungumzo" huko Jeddah kati ya jeshi la Sudan na Vikosi vya Msaada wa Dharura(RSF).
Siku ya Ijumaa ripoti zilisema mapigano yanaendelea huko Khartoum.
Jeshi la Sudan linasema kuwa mazungumzo hayo yanalenga kushughulikia masuala ya kibinadamu.
RSF haijatoa kauli rasmi kuhusiana namazungumzo hayo.
Jeshi lilithibitisha kuwa limetuma wajumbe huko Jeddah kushiriki katika mazungumzo hayo, ambayo Umoja wa Mataifa na mashirika ya misaada yamekuwa yakishinikiza, yakikabiliwa na mzozo mbaya wa kibinadamu nchini Sudan.
Wiki tatu za mapigano makali yamesababisha vifo vya mamia ya watu na kuwafanya raia 450,000 kuyahama makazi yao.
Shirika la Kimataifa la Uhamiaji linasema, zaidi ya watu 115,000 wametafuta hifadhi katika nchi jirani.
Kamanda wa jeshi la Sudan Jenerali Abdel Fattah al-Burhan - rais halisi wa Sudan - yuko katika mzozo mkali wa madaraka na kiongozi wa RSF Jenerali Mohamed Hamdan Dagalo, kwa jina maarufu Hemedti.