Ndege ya Uturuki iliyokuwa ikitua katika kambi ya anga nje ya mji mkuu wa Sudan, Khartoum, imeshambuliwa, wizara ya ulinzi ya Uturuki imethibitisha.
Hakuna aliyejeruhiwa na ilitua salama Wadi Seidna, ambako ilikuwa ikikaguliwa. Jeshi la Sudan limewalaumu wapiganaji wa RSF kwa kufanya shambulio hilo na kuharibu mfumo wake wa mafuta.
Vikosi vya RSF vinavyopambana na Jeshi la serikali vilikanusha madai hayo, vikisema kuwa vimejitolea katika kulinda haki za kibinadamu.
Muda wa kusitisha mapigano Sudan umerefushwa lakini mapigano yanaendelea
Taarifa kutoka Sudan, na kwingineko barani zinasema makundi hasimu ya kijeshi yalikubali kurefusha muda wa kusitisha mapigano usiku wa manane saa za huko (Saa 22:00 GMT siku ya Alhamisi) kwa siku tatu zaidi.
Makubaliano ya awali yaliruhusu maelfu ya watu kujaribu kuondoka kwa usalama nchini humo, huku mataifa kadhaa yakipanga kuondoa raia wao.
Waziri wa ulinzi wa Uturuki amesema juhudi zitaendelea kuwaokoa raia wa Uturuki kutoka Wadi Seidna na mji wa Port Sudan kwenye pwani ya Bahari Nyekundu.
Tangu mapigano hayo yaanze siku 14 zilizopita, mamia ya watu wameuawa na makumi ya maelfu kulazimishwa kuyakimbia makazi yao.