Simba inapaswa kuwa na nidhamu kubwa hasa ya kujilinda ili kuhakikisha Al Ahly hawana madhara makubwa kwao na wao waweze kupata matokeo mazuri yatakayowavusha.
Uimara wa hali ya juu unapaswa kuwepo katika safu ya kiungo ambayo imekuwa ikifanya makosa ya mara kwa mara ya kuruhusu wapinzani kumiliki mpira na kutengeneza nafasi, jambo linalopelekea safu ya ulinzi ishambuliwe mara kwa mara.
Wawakilishi hao wa Tanzania wanapaswa kutimiza wajibu kitimu hasa kukaba na kutafuta mpira pindi unapokuwa kwa Al Ahly, jambo ambalo litawanyima uhuru wapinzani wao katika kutengeneza hatari kwao.
Kuepuka makosa binafsi ya kiulinzi kunaweza kuwa msaada mkubwa kwa Simba ambayo siku za hivi karibuni imeonekana kuruhusu idadi kubwa ya mabao kutokana na uzembe binafsi.