Baada ya kuota mbawa mechi ya Simba na Coastal Union ambayo iliombwa ichezwe kesho kutwa Ijumaa, mastaa wa timu hiyo wamepewa mapumziko ya siku nne kuanzia leo Jumatano na watarejea kambini Jumapili.
Simba iliandika barua Bodi ya Ligi Kuu (TPLB) ili mechi hiyo ya raundi ya tatu ya Ligi Kuu ambayo haijapangiwa tarehe ili ichezwe kupunguza viporo lakini baadaye bodi hiyo haikujibu maombi hayo. Awali kupitia Afisa Habari wa Simba, Ahmed Ally alisema wamekubaliwa mechi hiyo ichezwe lakini baadaye makubaliano hayo yaliota mbawa.
Tayari Simba baada ya mechi yao na Dodoma Jiji iliyochezwa Uwanja wa Uhuru, Jumapili na kuibuka na ushindi wa mabao 2-0 juzi Jumatatu timu hiyo iliingia kambini kujiandaa na mechi yao na Wagosi wa Kaya ambapo jana baada ya bodi kusisitiza ratiba kutokuwa na mabadiliko yoyote kocha Robertinho aliamua kuwapa mapumziko wachezaji.