Serikali imesema jitihada za uokoaji kutokana na mafuriko wilayani Hanang, mkoani Manyara zinaendelea, ambapo tayari Jeshi laWananchi wa Tanzania (JWTZ) lipo katika hatua mbalimbali za kusaidia.
Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Queen Sendiga akizungumza eneo la tukio Katesh wilayani Hanang, amesema pia Timu kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu kitengo cha Maafa imeshawasili Hanang kwa ajili ya kushiriki kwa namna mbalimbali katika tukio hilo.
Amesema kuna nyumba ambayo imezingirwa na maji na watu wapo juu yap aa, hivyo itatumika helkopta kusaidia uokoaji.
Watu 23 wameripotiwa kufa, huku 30 wakijeruhiwa kutokana na mafuriko yaliyosababishwa na mvua kubwa iliyonyesha Katesh wilayani Hanang mkoani Manyara kuanzia saa mbili usiku wa kuamkia leo Desemba 3, 2023.
“Uokoaji unaendelea, lakini pia jitihada za kutoa tope katika makazi ya watu, maeneo ya biashara na barabarani nazo zinaendelea,” amesema RC Sendiga.