Kocha Mkuu wa Yanga, Nasreddine Nabi, ameweka wazi kuwa, mikakati yake ni kuvuna alama tatu kwenye mechi yao ya leo Jumatano dhidi ya Real Bamako, itakayochezwa Uwanja wa Mkapa, Dar, huku mifumo mitatu ikianikwa.
Wakati Nabi akisema hayo, wachezaji wa kikosi hicho wakiongozwa na Fiston Mayele, wameweka wazi namna ambavyo wanavyoupa umuhimu zaidi mchezo huo wakiwataka mashabiki kujitokeza kwa wingi uwanjani.
Ofisa Habari wa Yanga, Ally Kamwe, alisema, kwenye kikao cha mwisho ambacho wamefanya kabla ya mchezo huo wa Kundi D katika Kombe la Shirikisho Afrika, Kocha Nabi aliainisha mbinu tatu za kuwamaliza Bamako.
“Kocha Nabi alisema wazi kuna mbinu tatu ambazo mashabiki wataziona kwa Mkapa Jumatano, lakini zote zikibebwa na kulishambulia kwa nguvu lango la Bamako.
“Yaani watashambuliwa kuanzia mwanzo hadi mwisho, huku kelele za mashabiki zikiwavuruga na hapo ndiyo watajua ukubwa ya Yanga. Lazima Bamako wapigwe kwa Mkapa,” alisema Kamwe.
Kwa upande wa Mayele, alisema, wanataka kwenda robo fainali, kutolewa kwenye hatua ya makundi ni jambo ambalo litakuwa baya kwao.
“Wananachi wajue kuwa sisi wachezaji tunataka ushindi kwenye mchezo huu, tunataka kwenda robo fainali na ili kwenda huko tunataka alama tatu, tutashinda kwa uwezo wa Mungu,” alisema.