Kocha Msaidizi wa Klabu ya Simba, Juma Mgunda amefunguka kuhusu kiungo wa timu hiyo, raia wa Ghana, Augustine Okrah kumalizana na Simba na kuondoka Klabuni hapo.
Mgunda amesema kuanzia sasa Okrah sio mchezaji tena wa Simba na hawatamtumia tena kwenye ichezo iliyosalia kumalizia Ligi.
“Ukweli ni kwamba Simba tayari wameshamalizana na mchezaji Okrah, pamoja na kwamba ni majeruhi na asingeweza kucheza kwa sababu ya majeruhi yake, lakini tayari ameshamalizana na klabu na si mchezaji wa Simba tena.
“Nilitaka niliweke hili sawa ili lisije kuleta sintofahamu. Okrah na Simba wamepatana kama walivyopatana na wameelewana kwa hiyo tunamtakia kila la kheri huko aendako,” amesema Mgunda.
Okrah ambaye alijiunga na Simba mwanzoni mwa msimu huu akitokea Bechem United ya Ghana na kuonyesha uwezo mkubwa lakini baadaye aliporomoka kiwango kutokana na majeruhi na sasa ameshapewa mkono wa kwaheri.
SImba itakuwa dimbani kesho Jumanne, Juni 6, 2023 kucheza na Polisi Tanzania katika Dimba la Chamazi Dar.