Kikosi cha Kaizer Chefs ya nchini Afrika Kusini kimewasili jijini Dar es Salaam usiku wa kuamkia leo kwa ajili ya mchezo wa kirafiki zidi ya Yanga SC wakati wa sherehe za kilele cha WIki ya Mwananchi.
Mchezo huo utachezwa kesho Julai 22, majira ya saa 1:00 jioni 2023 katika Dimba la Benjamin Mkapa.
Pamoja na mambo mengine klabu ya Yanga hutumia siku hii kutambulisha wachezaji wapya na wa zamani
Akizungumzia ujio wa Kaizer Chiefs, Ofisa Habari Yanga, Ally Kamwe amesema; "Wiki ya Mwananchi inakusanya mambo makubwa mawili, kwanza ni burudani ya mchezo wenyewe lakini burudani ya muziki kutoka kwa wasanii mbalimbali.
"Kwenye mchezo, tumeileta moja ya timu kubwa barani Afrika, Kaizer Chiefs ambao wataingia Dar es Salaam saa 8 usiku kuamkia Ijumaa Julai 21, 2023.
"Kaizer Chiefs kuja kucheza kwenye tamasha la kilele cha Wiki ya Mwananchi maana yake mchezo huu wa kirafiki wa kimataifa una hadhi ya Robo Fainali au Nusu Fainali ya CAF.
"Kwa hiyo mtu atakaekuja siku ya Jumamosi kwenye kilele cha Wiki ya Mwananchi atakata kiu ya mechi kubwa," amesema Ally Kamwe.