Michezo

Habari

Burudani

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Ijue rekodi ya Simba Day kwa miaka 15

Mashabiki SImba K 1 1140x640 Mashabiki wa Simba

Sun, 6 Aug 2023 Chanzo: www.tanzaniaweb.live

Ni msimu wa 15 tangu kuanzishwa kwa Tamasha la Simba Day mwaka 2009, chini ya Mwenyekiti wa Simba, Hassan Dalali.

Lengo lilikuwa kupata fedha za kujenga uwanja wa Bunju, wanachama wao kutambuana, kufanya shughuli za kijamii, kutambulisha wachezaji na jezi.

Mara ya kwanza kuifanya Simba Day, ilikuwa Agosti 8, mwaka 2009 viongozi na wanachama walikwenda Hospitali ya Taifa ya Muhimbili na kutoa mashuka 100 katika wadi ya watoto.

Siku hiyo Simba ilicheza  dhidi ya Sport Villa ya Uganda na  ilishinda 1-0, bao la kiungo Mkenya, Hilary Echessa.

Mwanaspoti linakuletea matamasha 14 ya ya Simba tangu tamasha hilo lilipoasisiwa chini ya uongozi wa Mzee Hassan Dalali na Mwina Kaduguda. Simba imeshinda matamasha tisa, ikipoteza manne na moja.

2009- Simba 1-0 SC Villa

‘Simba Day’ ya kwanza ilivaana na SC Villa ya Uganda. Katika mechi hiyo iliyopigwa Uwanja wa Uhuru (enzi (Uwanja wa Taifa) Simba ilishinda bao 1-0.

Simba ilikuwa chini ya Kocha Mzambia, Patrick Phiri. Na ndiyo msimu ambao Simba ilitwaa ubingwa bila kufungwa, huku nyota wa Uganda, Emmanuel Okwi na Joseph Owino wakisajiliwa kwa mara ya kwanza.

2010- Simba 0-0 Express

Mwaka wa pili Simba iliadhimisha kwa suluhu dhidi ya Express ya Uganda na mechi ilipigwa Uwanja wa Uhuru.

Bado Simba ilikuwa chini ya Kocha, Patrick Phiri na iliundwa na nyota kama Ally Mustafa ‘Bathez’, Owino, Mohamed Banka, Rashid Gumbo, Okwi, Patrick Ochan, Shija Mkina, Amri Kiemba na Mussa Hassan Mgosi na Jerry Santo.

2011- Simba 0-1 Victors

Hii pia ilikuwa timu kutoka Uganda, safari hii ilikuwa Victors na mechi ilipigwa Uwanja wa Sheikh Amri Abeid, Arusha. Kwa mara ya kwanza Simba ilipoteza mchezo kwa kulala bao 1-0. Bao hilo liliwekwa kimiani dakika ya 70 kwa mkwaju wa penalti na Patrick Sembuya. Kocha wa Simba alikuwa Mserbia Milovan Cirkovic.

2012- Simba 1-3 Nairobi City Stars

Wekundu wa Msimbazi chini ya Cirkovic waliteseka kwenye tamasha hili la nne baada ya kulala 3-1 kutoka kwa Nairobi City Stars ya Kenya.

Pambano hilo la msimu wa nne lilipigwa kwenye Uwanja wa Benjamini Mkapa na mabao ya washindi yakiwekwa kimiani na Duncan Owiti dakika ya 57, Bruno Okullu dakika ya 69 na Boniphace Onyango aliyehitimisha dakika ya 79, huku bao la kufutia machozi la Simba likiwekwa kimiani na Mzambia, Felix Sunzu katika dakika ya 15.

2013- Simba 4-1 SC Villa

Mwaka wa tano Simba iliialika tena SC Villa na kuishindilia mabao 4-1. Pambano lilipigwa Uwanja wa Taifa (Benjamin Mkapa), Simba ilikuwa chini Kocha Abdallah Kibadeni aliyechukua nafasi ya Cirkovic na chipukizi wa kipindi hicho, Jonas Mkude alifungua pazia kwa bao la dakika ya 43 kabla ya William Lucian ‘Gallas’ naye kuongeza la pili dakika ya 53. Mkongwe Betram Mombeki aliyefunga mawili dakika ya 70 na 72.

2014- Simba 0-3 Zesco

‘Tanesco’ ya Zambia, Zesco FC ilifanya kufuru kwa kuitibulia Simba sherehe kwenye tamasha la sita kwa kuinyoosha kwa mabao 3-0, enzi hizo timu ikiwa chini ya Kocha Mcroatia Zdravko Logarusic. Mabao hayo yalifungwa na Jackson Mwanza dakika ya 14, Clatus Chama dakika ya 64 kwa penalti na Mayban Mwamba dakika ya 90.

2015- Simba 1- 0 SC Villa

Tamasha la saba ya Simba Day liliishuhudia SC Villa ikirudi tena kwa mara ya tatu na ilifungwa bao 1-0.  Bao la Awadh Juma dakika ya 89.

2016- Simba 4-0 AFC Leopards

Katika tamasha la nane Simba ilipata ushindi dhidi ya AFC Leopards ya Kenya kwa mabao 4-0. Ibrahim Ajibu alifunga mawili na Mrundi, Laudit Mavugo la tatu na Shiza Kichuya alifunga la nne.

2017- Simba 1-0 Rayon Sports

Tamsha la tisa Simba ilitakata kwa dhidi ya Rayon Sports ya Rwanda bao 1-0 la kiungo, Mohammed Ibrahim dakika ya 15 asisti ya Emmanuel Okwi.

2018- Simba 1-1 Asante Kotoko

Tamasha la 10, Simba ilicheza na timu kutoka nje ya Afrika Mashariki baada ya Zesco ya Zambia (2014). Simba ilishindwa kutamba dhidi ya Asante Kotoko ya Ghana baada ya kufungana bao 1-1 kwenye Uwanja wa Taifa.

Simba 3-1 Power Dynamos (2019)

Tamasha la 11 Simba iliibuka na ushindi wa mabao 3-1 dhidi ya Power Dynamos kutoka Zambia huku Meddie Kagere akipiga hat-trick.  Simba chini Rais Evans Aveva, aliliboresha tamasha na kuwa Wiki ya Simba na kufanya mambo mbalimbali.

Simba 6-0 Vital’O (2020)

Tamasha la 12, Simba iliibukana ushindi mkubwa. Msanii mkubwa wa Tanzania Diamond Platnams alitua na helikopta. Mabao ya Simba yalifungwa na Bernard Morrison, John Bocco, Clatous Chama, Ibrahim Ajibu, Chris Mugalu na Charles Ilamfya.

Simba 0-1 TP Mazembe (2021)

Tamasha la 13, halikuwa zuri kwa Simba kwani ilikubali kichapo cha bao 1-0 dhidi ya wageni TP Mazembe. Bao la tik-taka la Jean Baleke ambaye kwa sasa anakipiga Simba.

Simba 2-0 St George (2022)

Tamasha la 14, lilikuwa zuri kwa Simba kwani ilirudisha matumaini kwa ushindi wa mabao 2-0 mabao ya Denis Kibu na Nelson Okwa. Tamasha lilipambwa na msanii wa WCB, Zuhura Othuman Soud.

2023- Simba v Power Dynamos

Itakuwa mara ya pili kwa Power Dynamos kualikwa kwenye tamasha hili, mwaka 2019 ilifungwa 3-1. Pambano hilo la leo Agosti 6 linasubiriwa kwa hamu kwa sababu timu hizo zinaweza kukutana tena kwenye hatua ya pili Ligi ya Mabingwa Afrika lakini kingine ni mgeni rasmi wa tamasha la mwaka huu anatarajiwa kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan.

Chanzo: www.tanzaniaweb.live
Related Articles: