Rais wa Klabu ya Yanga, Eng. Hersi Said amewapongeza mashabiki wa klabu hiyo kwa kuendelea kuisapoti timu hiyo na kufanikisha kufikia hatua ya robo fainali ya Kombe la Shrikisho Barani Afrika baada ya kuichapa US Monastir ya Tunisia na kufikisha alama 10.
Hersi ambaye alianza mwakilishi wa mdhamini wa Yanga, GSM na kuhusika kwa asilimia kubwa katika kusaka wachezaji na kuwasajili katika kikosi hicho kisha kuwania urais wa Yanga na kushinda, amesema hayo jana wakati akihojiwa na wanahabari baada ya mchezo huo kumalizika.
“Ninamshukuru Mungu kwa hiki kilichotokea leo, kwangu mimi naona ni jambo kubwa. Ninawashukuru sana Wanayanga kwa nguvu waliyoionyesha kuisapoti timu yao mpaka leo tunaona tumepata matokeo. Wameisapoti timu katika matokeo mazuri na mabaya na leo timu imeingia robo fainali.
“Safari bado haijakwisha, tulikuwa na malengo ya kuingia kwenye makundi, tumevuka makundi na leo tumeingia robo fainali. Kama nilivyosema, safari haijaisha, twendeni tukaisapoti timu kwenye robo fainali. Huwezi kujua inaweza kuwa nusu fainali, inaweza kuwa fainali, au ubingwa,” amesema Hersi.