Baada ya Jana Agosti 13 Simba kubeba Ubingwa wa Ngao ya Jamii 2023 mbele ya watani zao Yanga, mengi yameibuka hasa baada ya mshindi wa mchezo huo kupatikana kwa njia ya matuta.
Simba ilishinda kwa Penati 3-1, lakini malalamiko yalikuja pale ambapo ilisemekana mlinda mlango wa Timu ya Simba Ally Salim alikuwa akitoka eneo la goli kabla ya Penati kupigwa.
Sasa Mchambuzi wa michezo kutoka Clouds Fm, Edgar Kibwana kupitia ukurasa wake wa Instagram ameandika;
"Ally Salim anastahili pongezi nyingi kwa kile alichokionyesha katika mchezo dhidi ya Yanga, kudaka penalty 3 dhidi ya wana fainali sio mchezo.
Lakini kuna jambo ambalo halikua sawa kwa upande wa waamuzi ambao ndio wenye jukumu la kusimamia sheria zote uwanjani.
Kikawaida Golikipa wakati wa kudaka penalty hapaswi kutoa miguu yake yote kabla mpigaji hajapiga mpira lakini kwa Ally Salim ilikuwa tofauti, alikua anatoka hata kabla mpira haujapigwa.
Katika penalty zote tatu alizocheza zilistahili kurudiwa kwani zilikuwa zinapigwa wakati ambao ameshatoka kwenye mstari".