Wanafunzi wapatao 15 wa shule ya Sekondari Naura katika Kata ya Lemara Jijini Arusha, wamekutwa na visu na misokoto ya bangi wakiwa wamejificha ndani ya mto Themi eneo la mtaa wa Engosengiu kata ya Sinoni, muda ambao walitakiwa kuwa darasani.
Aidha, Mgambo wa kata, viongozi wa mtaa na wananchi, inadaiwa wakiwa wanajaribu kuwakamata wanafunzi hao, walianza kutishiwa kuchomwa visu na kundi hilo, ambapo baadae wanafunzi watatu walikamatwa na wengine kukimbilia kusikojulikana.
Diwani wa kata ya Sinoni, ndugu Michael Kivuyo amethibitisha kutokea kwa tukio hilo katika eneo lake, na kusema zinahitajika jitihada za haraka kwakua kundi hilo ni hatarishi kwenye Jamii.
Uongozi wa shule hiyo umesema umesikia taarifa hiyo kutoka kwa wananchi na wanasubiri kuletewa taarifa zaidi ili wawatambue wanafunzi hao.