Samia Mohamed (20), mkazi wa Kijiji cha Sinde, Kata ya Msangamkuu Wilaya ya Mtwara mkoani Mtwara amefariki dunia kwa kile kinachodaiwa kuwa amenyongwa.
Akizungumza leo mkoani Mtwara, Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa Mtwara, Mtaki Kurwijila, amesema marehemu ambaye ni mlemavu wa miguu na mikono, alikutwa akiwa amefungwa kamba ya manila shingoni kama mtu aliyejinyonga pembeni mwa jiko nyumbani kwao.
"Katika upelelezi wa awali imebainika kwamba kutokana na ulemavu wa mikono na miguu aliyokuwa nao marehemu, uwezekano wa kujinyonga ni mdogo sana," amesema Kurwijila na kuongeza kuwa mwili wa marehemu umehifadhiwa katika Hospitali ya Rufaa Ligula mkoani humo kwa ajili ya kufanyiwa uchunguzi wa kitabibu.