Jeshi la Polisi mkoani Mwanza, linamshikilia Said Mfaume (32), akidaiwa kumjeruhi mapenzi wake, Faudhia Juma (24) kwa kumchoma kisu maeneo mbalimbali ya mwili wake, kisha naye kujichana tumboni kwa madai kuwa mwanamke huyo amekataa kuolewa naye.
Taarifa hiyo imetolewa leo kwa waandishi wa habari na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza, Wilbroad Mutafungwa, ambapo amesema tukio hilo lilitokea Agosti 6, mwaka huu katika nyumba ya kulala wageni ya Citizen Lodge, iliyopo eneo la Pasiansi wilayani Ilemela mkoani Mwanza.
Kamanda Mutafungwa amesema mwanaume huyo ambaye ni Mtaalam wa Teknolojia ya Habari (IT), baada ya kupata taarifa kuwa mwanamke huyo amekataa kuolewa naye, na kwamba katoroka nyumbani kwao mkoani Singida, alimfuatilia na kubaini kuwa yuko Mwanza.
"...Baada ya kubaini yuko Mwanza alimwita kwenye Lodge hiyo ndipo alipomshambulia kwa kutumia kisu maeneo mbalimbali ya mwili wake," amesema Mutafungwa.
Kamanda Mutafungwa amesema mtuhumiwa baada ya kumshambulia mpenzi wake na kuamini amemuua, alijichana tumbo kwa kutumia kisu na kufanya utumbo uning'inie jambo lililosababisha apoteze fahamu kabla ya maofisa wa Polisi kupata taarifa na kuwapeleka Hospitali ya Mkoa ya Sekou Toure kwa matibabu.
"Faudhia amepatiwa matibabu sekou Toure na kuruhusiwa kwenda nyumbani lakini mtuhumiwa kwa sababu alipata majeraha makubwa anaendelea kutibiwa chini ya ulinzi wa maofisa wa Polisi, afya yake ikitengemaa atafikishwa mahakamani," amesema.