Jeshi la Polisi mkoani Geita linamshikilia Flora Maplo (33), mkazi wa Kitongoji cha Amrima, Kata ya Rwamgasa, kwa tuhuma za mauaji ya mtoto wake mwenye umri wa miezi miwili.
Mtoto huyo anadaiwa kuuawa kwa kunyongwa shingo na kukatwa mkono wa kulia na mguu wa kulia kisha mwili kutelekezwa njiani.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Geita, Sofia Jongo, alithibitisha kutokea kwa tukio hilo ambalo alisema lilitokea Julai 22, mwaka huu, katika kitongoji cha Mienze, wilayani Bukombe.
Kamanda Jongo alisema hali ya mkoa huo ni shwari bali matukio machache yanayoendelea kutokea yanasababishwa na wananchi wenyewe kutokana na visasi, kuchukulia sheria mkono na imani potofu.
Katika hatua nyingine, Kamanda Jongo alithibitisha kujeruhiwa na kitu chenye ncha kali kwa binti Rehema Paul (26), Mkazi wa Kata ya Katente Wilaya ya Bukombe aliyejeruhiwa sehemu za kichwani na kukatwa viganja vyake viwili na mume wake kwa wivu wa mapenzi.
"Binti huyu alikuwa na bwana ambaye walikuwa na migogoro wa kimapenzi ambapo siku ya tukio alipigiwa simu na mtu akimtaka waonane sehemu na baada ya kufika eneo hilo alivamiwa na kuanza kushambuliwa," alisema Kamanda Jongo.
Aidha, alisema baada ya kutekeleza ukatili huo mwanamume huyo aliyetambulika kwa jina la Baba Lawi alitokomea kusikojulikana pamoja na mke wake na kuwa jeshi hilo linaendelea kuwasaka ili sheria ichukue mkondo wake.