Sara Robert (33), Mkazi wa Ilunda wilayani Sengerema mkoani Mwanza amehukumiwa kifungo cha mwaka mmoja gerezani baada ya kukutwa na hatia ya kuiba mtoto wa kiume mwenye umri wa miezi mitatu
Akisoma hukumu ya kesi hiyo ya jinai namba 72 ya mwaka 2023 katika Mahakama ya Wilaya ya Sengerema Hakimu mkazi Mwandamizi, Evodi Kisoka amesema hukumu hiyo imetolewa mara baada ya mshtakiwa kukiri kutenda kosa hilo.
Awali mwendesha Mashtaka wa Serikali ambaye ni Mkaguzi wa Polisi, Martha Chacha aliieleza mahakama hiyo kuwa mshtakiwa alitenda kosa hilo kinyume na Kifungu namba 169 (1) ( A) cha Kanuni ya Adhabu sura ya 16 toleo la mwaka 2022
Mwendesha mashtaka huyo wa serikali ameiambia mahakama hiyo kuwa mshitakiwa alitenda kosa hilo Januari 14, mwaka huu majira ya saa mbili usiku katika Kitongoji cha Nyankorongo kilichopo kijiji cha Nyamtelela wilayani Sengerema Mkoani humo kwa nia ya udanganyifu kwa kumuiba mtoto wa Mkazi wa Mtaa huo, Jesca Matiku.
Akitoa utetezi wake, mbele ya Mahakama hiyo, mshtakiwa Sara Robert akaiomba mahakama hiyo impunguzie adhabu kwa madai kuwa hakuwa na nia ovu ya kumdhuru mtoto huyo bali alitaka kuishi naye kwani hana mtoto wa kiume ili ainusuru ndoa yake na pia watoto wake ambao ni wa kike bado wanamtegemea.
Hata hivyo Mahakama ilitupilia mbali maombi yake hayo ikamhukumu kifungo cha mwaka mmoja gerezani ili iwe fundisho kwa watu wengine watakaojaribu kufnaya kosa kama lake la kuiba mtoto.