Mabingwa mara saba wa Kombe la Mataifa ya Afrika AFCON 2021 Misri wamefuzu kucheza hatua ya 16 bora ya michuano hiyo baada ya kuibuka na ushindi mgumu wa goli 1-0 dhidi ya Sudan katika mechi ya mwisho Kundi D ambapo sasa watamaliza na alama sita.
Misri ambao ndio wamebeba taji hilo mara nyingi zaidi, walikuwa wanahitaji alama moja tu kufuzu hatua ya mtoano lakini wakapata ushindi ambao umewapa uhakika zaidi kupitia bao la Mohamed Abdelmonem akimalizia mpira wa kona wa Abdallah El Said kunako dakika ya 35 ya mchezo.
Kutokana na matokeo hayo, Misri watakutana na kinara wa Kundi E Januari 26 ambapo kundi hilo linaundwa na timu ya Ivory Coast, Algeria, Sierra Leone na Equatorial Guinea.
Misri wamemaliza alama tatu nyuma ya vinara wa Kundi D kufuatia Nigeria kuongoza baada ya kuvuna ushindi wa goli 2-0 dhidi ya Guinea Bissau.