Kocha Mkuu wa Simba, Fadlu Davids amewataka mashabiki na wananchama wa timu hiyo kutokuwa na presha na kusahau kuhusu kipigo cha bao 5-1 walichokipokea msimu uliopita kutoka kwa watani zao, Yanga SC.
Fadlu ambaye amejiunga na Simba msimu huu amesema kuwa mchezo wa kesho wa Ngao ya jamii dhidi ya Yanga watauendea kama michezo mingine yoyote na kulingana na mipango yake pamoja na uwezo wa wachezaji wake, anaamini watapata ushindi.
"Nimezitazama mechi zote za dabi za msimu uliopita, ile ya bao 5-1 kipindi cha kwanza ni kama timu zote zililingana. Ile mechi ya bao 2-1, Simba walikuwa vizuri mwanzoni mwa kipindi cha kwanza, hakukuwa na utofauti mkubwa kwa timu zote mbili kwenye ubora wa mchezaji mmoja mmoja.
"Wachezaji wa Yanga wamekuwa pamoja kwa muda mrefu, ni faida kwao nah ii ni tofauti na sisi ambao takribani wachezaji wapya 14 utegemee wataweza kuelewana kwa muda mfupi, namna ya kuwasiliana uwanjani.
"Tuna timu mpya, Yanga hawawezi kujua nani ataanza kwetu, ni mpango gani tutaingia nao kwenye mchezo huo, kwa hiyo hiki ni faida kwetu, hata kama kocha wao atajaribu kubashiri kikosi chetu ataingia chaka tu," amesema Fadlu.