“Zamu ya nani? Ni zamu ya Namungo’ Ndivyo wanavyotamba mashabiki wa Yanga wakiwa na jeuri ya ushindi wakisisitiza kwamba wanarudi mzigoni kwenye Ligi Kuu, leo kuwakaribisha Namungo.
Timu zote zinakwenda kucheza mechi ya tatu katika ligi huku wenyeji Yanga wakiwa na ubora mkubwa kutokana na mfululizo wa vipigo vikali walivyoanza kutoa msimu huu ndani na nje ya nchi.
Katika mechi mbili za ligi ambazo Yanga imecheza sio tu imeshinda zote, lakini pia imezipiga KMC na JKT Tanzania kwa mabao 5-0 kila moja, ikiwa ndio timu iliyogawa vipigo vikubwa huku ikiwa haijaruhusu bao.
Ukiacha ubora wa Yanga rekodi inawabeba mabingwa hao watetezi wa ligi ambapo hawajawahi kupoteza mechi yoyote mbele ya Namungo.
Hakuna mchezaji ambaye Yanga itamkosa kwenye mchezo huo ambao utapigwa Azam Complex Chamazi kuanzia saa 1:00 usiku, huku nahodha Bakari Mwamnyeto akirejea kazini.