KOCHA Mwinyi Zahera anatarajiwa kurithi mikoba ya kocha Aristica Cioaba wa Azam FC aliyetupiwa virago juzi pamoja na kocha wa viungo, Costel Birsan, wote wakiwa raia wa Romania.
Taarifa kutoka kwa Mtendaji Mkuu wa klabu ya Azam, Abdulkarim Amin ‘Popat’ inasema tayari wamefanya mazungumzo na Zahera kwa ajili ya kushika jukumu la kuifundisha timu hiyo inayoshika nafasi ya pili katika msimamo wa Ligi Kuu Tanzania Bara.
“Ni kweli Zahera tumefanya mazungumzo naye na tumefikia makubaliano ya kuifundisha timu yetu, bado mambo madogo ili aanze kazi rasmi,” alisema Popat. Zahera ambaye baada ya kuondoka Yanga alikuwa Mkurugenzi wa Ufundi wa Gwambina FC atakuwa pamoja na kocha msaidizi, Bahati Vivier, kutoka Burundi.
Cioaba aliingoza Azam FC kwenye mechi 50 za mashindano (Ligi Kuu na Kombe la FA), akishinda mechi 28, sare 11 na kupoteza 11.
Awali aliiongoza Azam FC kuanzia Januari 10, 2017 hadi Mei 3, 2018 alipofukuzwa kabla ya kurejeshwa Oktoba 22, mwaka jana kufuatia kuondoka kwa Mrundi, Etienne Ndayiragijje aliyehamia timu ya taifa, Taifa Sta