Legendi wa Manchester City, Yaya Toure ameungana na akademi ya Tottenham na kuchukua majukumu ya kufundisha wakati akiwa anafanya masomo yake ya kuwa meneja.
Staa huyu wa zamani wa Manchester City, tayari alishawahi kuwa kocha nchini Urusi, lakini amerejea Uingereza kwa ajili ya kutafuta leseni ya UEFA (UEFA A-Licence).
Toure, anaishi Hampstead na kwa mujibu wa Evening Standard, staa huyu wa zamani mwenye miaka 38 alikuwa anatafuta klabu ambayo itakuwa karibu na mazingira yake ya nyumbani ili aweze kufanya nayo kazi.
Baada ya kukamilisha hatua za msingi, sasa nyota wa zamani wa Ivory Coast, Yaya Toure atakuwa akitumia siku kadhaa za wiki kwa ajili ya kuwafundisha vijana wa akademi ya Tottenham kwenye viwanja vya mazoezi vya Enfield.
Hata hivyo, staa huyu wa zamani hatakuwa akijihusisha na timu ya Tottenham ambayo iko chini ya Antonio Conte, na badala yake ataungana na meneja wa akademi Dean Rastrick pamoja na mkuu wa ukufunzi wa vijana Chris Powell.