Uongozi wa Yanga umeweka wazi kuwa unahitaji kupata matokeo mazuri dhidi ya Mtibwa Sugar ili waendelee kusalia kileleni mwa msimamo wa ligi kuu.
Yanga kesho Jumamosi wanatarajiwa kukipiga dhidi ya Mtibwa Sugar katika mchezo unaotarajiwa kufanyika katika Uwanja wa Manungu uliopo mkoani Morogoro.
Akizungumza na Championi Ijumaa, Meneja wa Yanga, Walter Harryson alisema kuwa malengo yao ni kuhakikisha kuwa wanaendelea kupata matokeo mazuri ili waendelee kuongoza ligi katika mzunguko wa pili ambapo melengo yao ni kuhakikisha kuwa wanatwaa ubingwa wa ligi.
“Tunamalengo ya kuhakikisha kuwa tunatwaaa ubingwa wa ligi kuu msimu huu, hivyo lazima tuhakikishe kuwa tunashinda na kupata matokeo katika kila mchezo ambao upo mbele yetu.
“Tunakwenda kucheza na Mtibwa Sugar tunafahamu ugumu wa mchezo huo kutokana na uzoefu wao katika ligi kuu lakini ili tuweze kuwa bora basi yatupasa kushinda katika kila mchezo ambao upo mbele yetu,” alisema kiongozi huyo.