Michezo

Habari

Burudani

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Yanga yashitukia michezo ya mawakala wa wachezaji

Fei Kamwe Yanga yashitukia michezo ya mawakala wa wachezaji

Mon, 24 Jun 2024 Chanzo: www.tanzaniaweb.live

Klabu ya Yanga imesema kuwa baadhi ya mawakala wanaitumia klabu hiyo kwa ajili ya kuwapa thamani wachezaji wao na kuwauza kwa dau kubwa.

Ofisa Habari wa klabu hiyo, Ali Kamwe, amesema baadhi ya mawakala wa wachezaji wamekuwa na tabia ya kuwahusisha wachezaji kuwa wanatakiwa na Yanga ili kuzifanya timu zingine zipande dau wakati si kweli kama wanawahitaji.

Kamwe alisema vitendo hivyo vilifanyika msimu uliopita na anashangaa msimu huu vimeibuka tena, akiwataka mawakala kuwauza wachezaji kwa thamani zao halisi na kuacha kuitumia Yanga kwa njia ya kuwapandisha thamani na kupata pesa nyingi za usajili.

"Mwaka jana hawa mawakala walitengeneza stori kuwa kuna mchezaji Yanga inamtaka, lakini alipokwenda klabu nyingine ikasemekana eti ameibiwa Uwanja wa Ndege, sisi wala hatukusema kitu," alisema Kamwe.

Ingawa hakufafanua, lakini ukirejea moja ya stori za matukio ya msimu uliopita ilisemekana kuwa Simba ilimpora mchezaji raia wa Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo, Fabrice Ngoma, Uwanja wa Kimataifa wa Ndege wa Julius Nyerere, akiwa anakuja kusaini mkataba Klabu ya Yanga.

"Kuelekea msimu unaokuja tunaanza kusikia tena habari kama zile, wanasema kuna kiungo tumepokonywa, si kweli ukiona hivyo hatukumhitaji, hivyo ni kazi ya mawakala kupiganisha ili wapige pesa," alisema Ofisa Habari huyo.

Hivi karibuni katika tetesi za usajili inadaiwa ilikuwa katika hatua za mwisho kumsajili kiungo mkabaji wa Singida Black Stars, Yusuph Kagoma, lakini taarifa zilizokuja baadaye zikaeleza, Simba imepindua meza na kumsainisha mkataba wa miaka mwili.

Hata hivyo, bado Simba haijathibitisha rasmi kumsajili mchezaji huyo mpaka sasa. Akizungumzia usajili, Kamwe alisema tayari wameshamaliza kazi iliyobaki ni kuwatangaza tu.

Tangu awali, Yanga ilitangaza kuwa haitofanya usajili mkubwa sana kwani bado ina kikosi imara, na ilichofanya ni kuzuia wachezaji wake muhimu kubaki, na kufanya usajili wa wachezaji wachache tu wenye viwango vya hali ya juu kwa ajili ya kukiongezea nguvu kikosi.

"Malengo tuliyonayo ni makubwa na usajili tulioufanya, watu watalia na kusaga meno," alisema Kamwe.

Tetesi zinadai kuwa Yanga imekamilisha usajili wa wachezaji, Emmanuel Bola Lobota, winga kutoka Singida Black Stars,  Agee Basiala, kiungo mshambuliaji kutoka  AS Maniema Union na beki wa kushoto, Chadrack Boka kutoka Klabu ya Saint Eloi Lupopo, wote hao kutoka DR Congo.

Mwingine ni kipa Khomein Abubakar wa Singida Black Stars, anayekwenda kuchukua nafasi ya Metacha Mnata, anayetajwa kuondoka msimu ujao.

Chanzo: www.tanzaniaweb.live