Michezo

Habari

Burudani

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Yanga yapokewa kifalme

39cc882a9cdfaa83aa261a3c2ee98803 Yanga yapokewa kifalme

Sun, 17 Jan 2021 Chanzo: habarileo.co.tz

MAMIA ya mashabiki wa klabu ya Yanga walijitokeza kwa wingi jana Bandarini Dar es Salaam kuipokea timu yao wakiwa na furaha na shangwe ikitokea Zanzibar ambako ilitwaa Kombe la Mapinduzi.

Yanga ilishinda kombe hilo baada ya kuifunga Simba kwa penalti 4-3 kufuatia suluhu katika dakika 90 za mchezo huo uliochezwa hivi karibuni kwenye Uwanja wa Amaan Zanzibar.

Mashabiki waliojitokeza kuilaki timu hiyo walikuwa wakicheza, wengine wakitazama na kupiga picha kwa furaha na baadhi wakiimba nyimbo za kukejeli watani zao wa jadi Simba wakionesha matumaini mapya baada ya misimu mitatu mfululizo kukosa Kombe lolote.

Kocha wa Yanga, Cedric Kaze alisema Kombe hilo ni mwanzo wa furaha na kuwataka mashabiki wajue kuwa wanarudi kazini ili waendelee kuwapa furaha furaha kubwa.

“Tunaamini kama huu ni mwanzo mashabiki wafurahi na wajue kuwa tuko imara tunaenda kurudi kazini ili kesho yake tupate furaha kubwa zaidi,”alisema.

Alisema anajua namna mzunguko wa pili wa Ligi Kuu Soka Tanzania Bara utakavyokuwa mgumu hivyo, wanapaswa kuwa makini katika maandalizi yao.

Kaze alisema kuna vitu watakwenda kufanyia kazi kuanzia kwenye benchi la ufundi hadi kwa wachezaji ili waweze kufanya vizuri zaidi. Nahodha wa kikosi hicho kilichoenda Zanzibar, Haruna Niyonzima alisema anaamini ubingwa walioupata ni ishara nzuri kwa Wanayanga hasa kutokana na muda mrefu kushindwa kupata mataji.

“Tumeanza vizuri na inaonesha kuna kitu ambacho kinakuja. Naamini kwa kikosi ambacho tunacho na ushirikiano tunaopewa kutoka kwa mashabiki, viongozi na benchi la ufundi tutapata taji msimu huu,”alisema.

Mkurugenzi wa Uwekezaji wa GSM, Hersi Said alisema wanafurahi kupata kombe hilo na kwamba katika dirisha dogo la usajili wameongeza mshambuliaji kutoka nje ya nchi na kwamba hakuna mchezaji yeyote ayakayeachwa. Alisema mchezaji huyo mpya atatambulishwa kwanza wakati wowote kisha atapokelewa wiki ijayo.

Chanzo: habarileo.co.tz