Kikosi cha Timu ya Yanga, kimeanza safari leo Jumanne, Februari 27, 2024 kuelekea nchini Misri kwa ajili ya mchezo wao wa mwisho wa hatua ya makundi ya Ligi ya Mabingwa Afrika dhidi ya Al Ahly.
Yanga na Ahly ambao wote wameshafuzu hatua ya robo fainali, watakipiga kwenye mchezo huo unaotarajiwa kufanyika Ijumaa, Machi 1, 2024 majira ya saa 1:00 nchini Misri.
Msafara wa watu 60 wakiwemo wachezaji 24, benchi la ufundi 13, watendaji na viongozi waandamanizi wa Yanga 23, kimeondoka Dar es salaam majira ya saa 11:55 jioni kuelekea Cairo nchini Misri kwa ndege ya Shirika la Ethiopia Airline.
Yanga wanatarajia kutua Addis Ababa Ethiopia kwenye Uwanja wa Bole majira ya saa 2:35 usiku, watapumzika kwa saa kama mbili hivi kisha saa 4:05 wataanza safari ya kutoka Ethiopia kwenda Cairo ambako watawasili saa 7:20 usiku (kuamkia kesho).