Michezo

Habari

Burudani

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Yanga na mapinduzi ya vijana

Hersi Rais Leo Yanga na mapinduzi ya vijana

Thu, 29 Dec 2022 Chanzo: Mwanaspoti

Yanga imejipanga kuendana na kasi ya ulimwengu unavyotaka, ambapo Sayansi na Teknolojia ndivyo vitu vinavyoshika kasi sana huku vijana wakiwa ndiyo tegemeo pekee la nguvu kazi ya taifa.

Hiyo ndiyo sababu ya kuweka rika hilo kuendesha klabu yao yenye makao yake Jangwani, Dar es Salaam ambayo miaka ya nyuma kwa kiasi kikubwa ilikuwa ikiongozwa na wakongwe.

Julai 9, mwaka huu, Yanga ilikuja na sura mpya baada ya wanachama kuwapa nafasi vijana kuiongoza, chini ya mwenyekiti wao, Mhandisi Hersi Said, alipokea kijiti kutoka kwa Mshindo Msola ambaye aliongoza kipindi kimoja (miaka minne).

Mwanaspoti linakuchambulia safu ya uongozi ya Yanga ambayo imeshikwa na vijana wenye nguvu wanaotaka kuendana na kasi ya soka jinsi zinavyoendeshwa klabu za kisasa duniani kote.

HERSI - RAIS

Kabla ya kupewa nafasi hiyo ya Rais, Hersi alikuwa Mkurugenzi wa Uwekezaji wa GSM ambayo ni sehemu ya uwekezaji wa Yanga, katika uongozi wake amefanikiwa kuchukua ubingwa wa Ligi Kuu Bara na Kombe la ASFC.

Yanga ilikaa miaka minne bila ubingwa ikishuhudia mataji yakitua Simba iliyobeba mara nne mfululizo.

Katika uongozi wake ameifanya timu hiyo kuingia makundi Kombe la Shirikisho Afrika, baada ya kuikosa nafasi hiyo kwa muda mrefu licha ya kutolewa Ligi ya Mabingwa.

ARAFAT - MAKAMU

Arafat Haji, kabla ya kuchaguliwa kumsaidia Hersi, aliwahi kuwa mjumbe wa kamati ya utendaji ndani ya klabu hiyo, nje na Wanajangwani ni Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Bima Zanzibar (ZIC).

Ni kijana mwenye nguvu za kutosha kuifanyia maendeleo Yanga, ikizingatia taaluma ya mambo ya fedha aliyonayo, pia katika nafasi ya ujumbe aliyoishika awali ilimpa uzoefu a kuiletea mafanikio.

Licha ya majukumu yake ya kikazi kuwa mengi, lakini amekuwa karibu na timu mpaka kusafiri nje ya nchi kila ambapo imekuwa ikienda katika michezo yao ya kimataifa.

Mbali na kuwa karibu na klabu ya wanaume, Arafat amekuwa akitoa mchango mkubwa kwa timu ya Yanga Princess ambayo amesimamia usajili wa msimu huu.

KAMWE - HABARI

Kabla ya kukabidhiwa ukuu wa habari ndani ya Yanga, Ally Kamwe ana uzoefu na nafasi hiyo kwani alikuwa mwanahabari katika vyombo tofauti hapa nchini pia mchambuzi wa soka.

Ujio wa Kamwe umeonyesha kitu tofauti na ilivyokuwa kutokana na namna ambavyo anaizungumzia timu yake muda wote na kuwajuza vitu vingi ambavyo vinawashawishi Wanayanga kuifutailia timu.

ALWATAN - MKUU WA MAUDHUI

Kutokana na uhodari wake wa kufanya kazi nzuri mitandaoni Yanga haikuchelewa kumchukua Abdulazeez Kipanduka ‘Alwatan’ ambaye amefanya kazi nzuri ya kuifanya klabu hiyo iwe nafasi ya pili kufuatiliwa zaidi mtandaoni mwezi uliopita (Novemba) tofauti na ilivyokuwa awali.

Alwatan ameleta mapinduzi kwani huko nyuma Simba ndiyo iliyokuwa inaongoza, ambapo kwa sasa inashika nafasi ya tatu, huku klabu ya kwanza ikiwa ni Al Ahly kutoka Misri.

GULAMALI - MJUMBE

Seif Gulamali ambaye ni mbunge kijana wa jimbo la Manonga naye amepata nafasi ya ujumbe wa kamati ya utendaji ili kuongeza nguvu ya kuhakikisha wanailetea maendeleo.

Gulamali ni kijana mwenye uwezo mkubwa katika uongozi baada ya kuisapoti timu yake akiwa nje akaingia ndani kushiriki kikamilifu. Wajumbe wengine wanaosaidia kuliendesha gurudumu hlo la Wanajangwani hao ni Alexander Ngai, Munir Said, Rodgers Gumbo na Everlist Yanga Makaga.

Chanzo: Mwanaspoti