Michezo

Habari

Burudani

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Yanga msiwachukulie poa Al Ahly

Ahly Tizi La Mwisho.jpeg Yanga msiwachukulie poa Al Ahly

Sat, 2 Dec 2023 Chanzo: www.tanzaniaweb.live

Wale Al Ahly hawajaisha kihiiivyo kama ambavyo watu hapa kwetu wanaaminishana wakati huu ambao mechi yao dhidi ya Yanga inakaribia kupigwa kesho Kwa Mkapa.

Tatizo watu wengi wa mpira hapa Tanzania huwa wanapenda kusikia wanayotaka kuyasikia yale ambayo hawataki kuyasikia ukiyasema wanakuchukia.

Hakuna sababu ya kutumia nguvu kubwa kuwabeza Al Ahly ili kuaminisha kuwa Yanga itapata ushindi katika mechi hiyo ya kesho na badala yake tusimame kwenye ukweli.

Ukweli ndio utaisaidia Yanga ijiandae vizuri na mechi ya kesho na sio kinyume chake kwani itajiona inaimudu Al Ahly na mwisho wa siku mambo yakaja kuwa kinyume watu wakaanza kutafutana maana ndio hulka ya soka letu.

Na naamini hata Yanga yenyewe inafahamu ugumu wa mechi dhidi ya Al Ahly na inafanya maandalizi makubwa kwa ajili ya mechi hiyo maana inafahamu fika kuwa ile watakayocheza nayo ndio bingwa mtetezi wa taji la mashindano hayo lakini ndio bingwa wa kihistoria kwa maana ya kutwaa mara nyingi taji la Ligi ya Mabingwa Afrika.

Ukubwa na mafanikio hayo ya Al Ahly ni vitu ambavyo havijapatikana kimiujiza au kushtukiza bali ni maandalizi mazuri na uwekezaji mkubwa ambao klabuĀ  hiyo imeufanya wa kuhakikisha inakuwa na timu nzuri na tishio kwa muda mrefu na ndicho tunachokiona hivi sasa.

Al Ahly ina wachezaji wengi wazuri kikosini ambao kundi kubwa ni nyota wanaozichezea timu tofauti za taifa Afrika ambao wana uzoefu wa kutosha wa mazingira tofauti ya bara letu lakini pia wana ubora mkubwa wa kutafsiri na kufanyia kazi kwa haraka na umakini mkubwa mbinu na mipango ya benchi la ufundi.

Wachezaji ambao wameshakutana na presha nyingi tofauti nje na ndani ya Misri hivyo wanajua nini wafanye ili wasiathirike nazo.

Jambo la msingi kwa Yanga ni kuingia ikiwa na morali kubwa na jitihada za hali ya juu huku ikiiheshimu Al Ahly kwa dakika 90 za mchezo vinginevyo ikijisahau itajuta baadaye.

Chanzo: www.tanzaniaweb.live