KLABU ya Yanga, imepania kuzoa pointi tatu kwenye mchezo wa Ligi Kuu Tanzania Bara dhidi ya JKT Tanzania unatarajiwa kuchezwa Uwanja wa Benjamini Mkapa Dar es Salaam leo.
Yanga wanaoshikilia rekodi ya kutopoteza mchezo na wanaongoza ligi kwa pointi 28 baada ya kucheza michezo 12 na kutoka sare minne wanakutana na wapinzani JKT ambao wapo katika nafasi ya 15 wakishinda michezo miwili, sare nne na kupoteza mechi sita.
Yanga wanahitaji ushindi kwenye mchezo huo ili kuendelea kujiweka kileleni na kuwa na tofauti ya pointi zilizopo kwa sasa dhidi ya Azam FC wenye alama 25 na Simba wenye pointi 23.
Yanga wataingia kwenye mchezo huo wakiwa na morali baada ya kushinda mchezo uliopita dhidi ya Azam lakini wanakutana na wapinzani wao ambao wamefanya vibaya kwenye mechi tano mfululizo.
Kocha wa Yanga, Cedric Kaze, alisema maandalizi yamekamilika na wachezaji wake wameandaliwa vya kutosha kupambana kama walivyofanya mchezo uliopita kuhakikisha wanapata ushindi.
“Kikosi kipo kwenye mazingira mazuri na hii inatokana na ushindi tuliopata kwenye mchezo uliopita, wana morali ya kupambana na kuendelea kutafuta ushindi ili tuendelee kujihakikishia kutawala kileleni,” alisema Kaze
Michezo mingine ya ligi itakayochezwa leo Dodoma Jiji yenye pointi 13 katika nafasi ya 13 itacheza dhidi ya Ihefu FC inayoshika mkia ikiwa na pointi sita mchezo kwenye Uwanja wa Jamhuri Dodoma.
Mbeya City yenye pointi 10 katika nafasi ya 16 watawaalika Mtibwa Sugar yenye pointi 12 katika nafasi ya 14 mchezo utakaofanyika Uwanja wa Kumbukumbu ya Sokoine Mbeya.