Shabiki maarufu wa Klabu ya Simba, anayefahamika kwa jina la Mchome amesema kuwa wachezaji wa timu hiyo hiyo hawajitumi uwanjani jambo linalosababisha kupata matokeo mabovu kila mchezo.
Mchome amesema hayo baada ya Simba kuwa na matokeo mabovu ambapo katika mechi tatu za mwisho kuanzia kipigo cha bao 5-1 kutoka kwa watani zao Yanga, sare ya bao 1-1 na Namungo na sare ya bao 1-1 na ASEC Mimosas ya nchini Ivory Coast katika michuano ya Ligi ya Mabingwa Afrika hatua ya makundi.
"Tangu tumepigwa bao 5 na Yanga zimekuja kuibua mambo mengi ambayo walikuwa wanaficha ficha. Yanga hakutufunga, alituonyesha udhaifu wetu. Viongozi walipaswa wachukue ile kama chachu ya mabadiliko lakini yaliyofuata ni yale yale, tukatoa sare na Namungo.
"Sare kwetu imekuwa kama ushindi, kama viongozi wameshindwa kuwadhibiti wachezaji waachie utawala wao waje watu wengine.
"Juzi hapa Che Malone alipata ajali akanusurika kuvunjika mguu alikuwa anatoka wapi saa 4 usiku? Watu wanasema alikuwa Kidimbwi kalewa, inamaana huyo mchezaji hayupo kambini," amesema Mchome.