Klabu ya Yanga SC imetangaza kusaini mkataba wa makubaliano na Kampuni za KILINET na N-Card kwa ajili ya kutengeneza kadi za kidigitali zitazokuwa zinatumiwa na Wanachama wa Klabu hiyo ambayo inaingia katika mfumo mpya wa uendeshaji, kadi moja itauzwa TZS 29,000.
Mkataba huo wa kampuni ya KILINET na klabu ya Yanga SC utahusisha masuala yote ya kidigitali ya klabu hiyo yanayohusiana na wanachama na utadumu kwa kipindi cha miaka mitano.
Tayari muonekano wa kadi hiyo umeoneshwa ambapo upande wa mbele una maelezo mbalimbali pamoja na picha na jina la Mwanachama huku upande wa nyuma ukiwa na picha ya jengo la Makao Makuu ya Yanga na kauli mbiu ya ‘daima mbele, nyuma mwiko’.
Faida moja wapo ya kuwa na kadi ya uanachama wa Yanga SC ni kuitumia kadi hiyo kuingia uwanjani na kufanya malipo ya serikali ikiwemo urahisi (Punguzo la bei) kwa baadhi ya huduma za wadau wa klabu hiyo.