Meneja mpya wa Barcelona, Xavi Hernandez ameanza vyema baada ya kuongoza kikosi hicho kupata ushindi mwembamba wa 1-0 dhidi ya Espanyol uwanjani Camp Nou.
Barcelona waliponea chupu chupu katika mechi hiyo iliyoshuhudia wageni Espanyol wakipoteza nafasi nyingi za kufunga mabao katika kipindi cha pili.
Bao la pekee na la ushindi kwa upande wa Barcelona lilipachikwa wavuni na Memphis Depay kupitia penalti ya dakika ya 48.
Ushindi wa Barcelona umewaweka katika nafasi ya sita kwa alama 20, nane nyuma ya Sevilla na Real Sociedad walio kileleni mwa jedwali.
Xavi alichezea Barcelona mechi 767 na akawaongoza kutia kapuni mataji 25 katika kipindi cha miaka 17. Hadi aliporejea Uhispania kuinoa Barcelona, Xavi alikuwa akinoa kikosi cha Al Sadd nchini Qatar.
Barcelona watavaana na Benfica ya Ureno nyumbani Camp Nou katika mchezo ujao wa Klabu Bingwa Ulaya (UEFA).