Straika wa KMC Wazir Junior amesema utulivu na kufuata maelekezo ya kocha ndiyo vimemfanya aweze kupachika mabao mawili kwenye mchezo dhidi ya Simba.
Junior alifanikiwa kufunga mabao hayo kwenye sare ya 2-2, katika mchezo uliopigwa kwenye Uwanja wa Chamazi.
Junior ambaye si mara ya kwanza kuifunga Simba, amesema kabla ya kuanza mechi hiyo kocha wake alimwambia kwa ubora wa wapinzani wao, atulie na asicheze kwa papara.
"Mabeki wa Simba ni wazuri, kufunga mabao mawili nilizingatia sana alichonisisitiza kocha kwamba nisiwe na papara,"amesema na kuongeza;
"Siyo mara ya kwanza kuifunga Simba, nimeifunga Mwanza nikiwa na Mbao, nikiwa na Toto Africa, nimeifunga Uwanja wa Benjamin Mkapa na leo hapa Azam Complex."
Straika huyo amefikisha mabao saba kwenye Ligi Kuu Bara msimu huu, jambo lililomfanya aone ana nafasi ya kuwania kiatu cha ufungaji bora.
"Kiatu cha mfungaji bora kipo wazi kwa kila mchezaji anayejituma na kufunga, bado mechi zimebaki nyingi, kazi yangu ni kufunga nitaendelea kupambana,"amesema.