Michezo

Habari

Burudani

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Wapinzani wa Simba kutua leo

586030411c40e8647d3d07b8bbc41c31.jpeg Wapinzani wa Simba kutua leo

Tue, 26 Jan 2021 Chanzo: habarileo.co.tz

WASHINDANI wa Simba katika michuano ya Super Cup wanaanza kutua leo tayari kwa mchezo wa kwanza utakaofanyika kesho kwenye Uwanja wa Benjamin Mkapa, Dar es Salaam.

Kwa mujibu wa mtandao wa Simba, timu ya kwanza kutua leo ni Al Hilal kutoka nchini Sudan, ambayo itawasili saa 7:00 mchana na jioni itafanya mazoezi tayari kwa mchezo huo wa kesho dhidi ya wenyeji wao.

Mbali na Al Hilal na Simba, timu nyingine itakayoshiriki mashindano hayo, ambayo ni mahususi kuwapatia mazoezi wawakilishi hao wa Tanzania katika Ligi ya Mabingwa wa Afrika, ni TP Mazembe ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo.

Simba iko katika Kundi A pamoja na AS Vita ya Congo, El-Merreikh ya Sudan pamoja na Al Ahly ya Misri katika Ligi ya Mabingwa wa Afrika. TP Mazembe na Al Hilal ya Sudan wenyewe wako katika Kundi B katika michuano hiyo ya Afrika.

Aidha, kocha wa Simba, Didier da Rosa amesema wachezaji wengi wa timu hiyo hawana utimamu wa mwili, hivyo kazi atakayoanza nayo ni kuwaweka fiti. Didier ambaye ni raia wa Ufaransa alitoa kauli hiyo siku moja baada ya kutambulishwa rasmi kama kocha mpya wa klabu hiyo kwa mkataba wa miaka miwili akirithi mikoba ya Mbelgiji, Sven Vandenbroeck.

Alisema licha ya kwamba aliwaongoza wachezaji wachache kwenye mazoezi siku hiyo ya kwanza, lakini amebaini kuna changamoto kwenye utimamu wa mwili, hivyo ni kitu ambacho ataanza kukifanyia kazi.

Didier alisema anajua Simba inahitaji kufika mbali zaidi ya ilipo na ina michuano migumu mbele, hivyo mchezaji akikosa utimamu wa mwili hana uwezo wa kushindana na mpinzani.

Alisema ameingia kwenye kikosi hicho wakati mzuri kwani kuna mashindano ya Simba Super Cup atakayoyatumia kujua uwezo wa wacheza kabla ya kupata kikosi chake cha kwanza.

Pia alishangazwa mashabiki wa Simba kujitokeza kwa wingi kushuhudia mazoezi ya timu hiyu akisema kuwa amezunguka ligi nyingi Afrika hajawai kuona upendo mkubwa wa namna hiyo.

Didier amejiunga na Simba baada ya kuvunja mkataba na miamba ya Sudan Al-Merrikh SC ambayo imemteua kocha raia wa Serbia, Miodrag Jesic kuwa kocha mkuu.

Chanzo: habarileo.co.tz