Michezo

Habari

Burudani

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Wakongwe wakubali mziki wa Simba SC

Simba1 Pic Data Juma Mgunda ndio Mwalimu wa Simba kwa sasa

Tue, 13 Sep 2022 Chanzo: www.mwanaspoti.co.tz

Mastaa wa zamani wa Simba, wamesema Simba ya sasa ni moto mkali na hii ni kutokana na nyota wake kubadili upepo kutoka kukejeliwa hadi kuwa mashujaa baada ya juzi kushinda ugenini dhidi ya Nyasa Big Bullets ya Malawi katika Ligi ya Mabingwa Afrika.

Kipa aliyezidakia Yanga, Simba na Mtibwa Sugar, Steven Nemes alisema kitendo cha timu hiyo kutoka sare ya kufungana mabao 2-2 dhidi ya KMC, mchezo wa Ligi Kuu Bara kuliwasaidia kujua tatizo lao, kisha wakarekebisha na kupata ushindi ugenini dhidi ya Wamalawi na sasa ni moto kwa namna ilivyocheza dhidi ya Malawi walioifumua mabao 2-0.

“Wakati mwingine makosa yanamtengeneza mtu kuwa bora, mfano Simba ikishinda mchezo na KMC, huenda wangejisahau na kuona wana kazi rahisi, lakini machungu yamewafanya waende wakihitaji umakini zaidi na ushindi,” alisema.

Kocha mkongwe, Abdallah Kibadeni alisema Simba imeanza vyema CAF, lakini akawakumbusha wachezaji kutojisahau kwa ushindi huo, badala yake wajiandae zaidi katika mchezo wa marudiano utakaopigwa Jumapili.

“Tayari zimeshasomana, ubora na pungufu ndio maana nawashauri na wajue mechi ya pili itakuwa ngumu zaidi, kwani wapinzani wao watakuja kivingine kwa kujua hawatakuwa na cha kupoteza,” alisema.

Beki wa zamani wa timu hiyo, Amir Maftah alisema ushindi ulioipata Simba umetuliza hasira za mashabiki waliokuwa hawaelewi kinachoendelea ndani ya timu hiyo, baada ya kuondoka kwa Zoran Maki.

“Ushindi unarejesha matumaini ya mashabiki kuamini timu inakuwa na taswira ya kufanya vizuri CAF na kwenye ligi ya ndani, kwani wao wanataka faraja tu na si jingine, hilo litaanza kuwarejesha uwanjani,” alisema.

Katika mechi hiyo ya juzi, Simba iliupiga mwingi hasa nyota wake, Moses Phiri, Clatous Chama na Ousmane Sakho.

Chanzo: www.mwanaspoti.co.tz