Michezo

Habari

Burudani

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Wachezaji Yanga kujazwa manoti

0fec0081ec2d86eaa7e7440a3476c524 Wachezaji Yanga kujazwa manoti

Sun, 17 Jan 2021 Chanzo: habarileo.co.tz

BAADA ya Yanga kurejea na Kombe la Mapinduzi mmoja wa wadhamini wao GSM ameahidi kuwapa wachezaji wote walioshiriki michuano hiyo na kurudi mashujaa zawadi nono.

Yanga ilitwaa ubingwa huo baada ya kuifunga Simba kwa penalti 4-3 katika mchezo wa fainali uliochezwa kwenye Uwanja wa Amaan, Zanzibar hivi karibuni.

Akizungumza baada ya kikosi hicho kurejea Dar es Salaam juzi, Mkurugenzi wa Uwekezaji wa GSM, Hersi Said alisema wachezaji hao ni wanaume katika wanaume kutokana na kile walichokifanya kwenye michuano hiyo.

“Sisi wadhamini Jumatatu tutakabidhi zawadi nono mashujaa wetu, “alisema na kuongeza kuwa wataendelea kushirikiana na klabu hiyo katika kujenga kikosi chenye ushindani.

Kwa upande mwingine, Kocha Mkuu wa kikosi hicho, Cedric Kaze aliwasifu wachezaji wake kwa kiwango kizuri walichokionesha katika michuano hiyo kwani wamefanya kazi yake ionekane rahisi.

“Kama una wachezaji wa hivi huwezi kuwa na kazi ngumu, tunajua bado hatujamaliza kazi, tunahitaji kupambana katika michuano ijayo ili tuifanye vizuri zaidi,”alisema.

Alisema kwa sasa mashabiki wa klabu hiyo wanaweza kutembea kifua mbele na kuvaa jezi zao kwani huko nyuma walikosa ujasiri kwa sababu ya kukosa kombe.

Kaze alisema huko waendako hawezi kuwahakikishia wanakwenda kuchukua taji la ligi ila anaweza kuwaahidi kutoa burudani nzuri.

Yanga inaongoza Ligi Kuu Tanzania Bara ikiwa na pointi 44 baada ya kucheza michezo 18 huku Simba ikishika nafasi ya pili ikiwa na pointi 35 ikiwa imecheza michezo 15.

Chanzo: habarileo.co.tz