Shirikisho la mpira wa miguu Tanzania TFF kwa kushirikiana na shirikisho la soka duniani ˜FIFA limehitimiza kozi ya awali kwa waamuzi 35 kutoka bara na visiwani Zanzibar wanaochezesha Ligi kuu kwa lengo la kuwajengea uwezo wa kutafsiri sheria 17 za soka.
Mkufunzi wa Waamuzi wa CAF nchini, Lesile Liunda amesema kozi hiyo iliyoanza Februari 24 mwaka huu hutolewa kila baada ya miezi 3 kwa awamu nne kwa msimu wa mwaka huu wa 2023.
''Tunawataka waamuzi mkatafsiri sheria 17 za mpira wa miguu vile inavyotakiwa na kuhakikisha mpira wa miguu unakuwa mchezo wa kiungwana kwa pande zote mbili kwani msimu mpya utakaoanza mwezi Agosti utakuwa mgumu na wa ushindani kutokana na timu zote kufanya usajili mzuri pamoja na maboresho mengi kwa timu zote; hivyo waamuzi mkawe sehemu ya kuifanya ligi yetu iwe bora na yenye kuvutia ili hata wadhamini wazidi kuongezeka.''Mkufunzi wa Waamuzi wa CAF nchini, Lesile Liunda
Nao Waamuzi ambao wameshiriki mafunzo hayo wamekiri mafunzo hayo yatawasaidia katika kazi zao za kutafsiri sheria 17 za mpira wa miguu na kupunguza makosa mbalimbali yanayolaumiwa na baadhi ya wadau wa soka nchini.
'naushukuru uongozi wa TFF kwa mapokezi mazuri na kwa kuandaa semina hiyo kwani imekuwa msaada mkubwa kwa waamuzi kujifunza.''
Miongoni mwa waamuzi ambao wamehudhuria mafunzo hayo ni pamoja na Mwamuzi Msaidizi maarufu, Frank Komba, Mwamuzi wa kati Ramadhani Kayoko, Heri Sasi na Mwamuzi mwanamama Jonisia Rukia.