LIGI Kuu ya Vodacom inaendelea kesho Jumamosi kwa viwanja sita kuwaka moto huku timu nyingi zikiwa na kumbukumbu za matokeo mabaya michezo iliyopita.
Coastal Union itakuwa nyumbani kucheza na Mwadui FC wakati Polisi Tanzania ikiikaribisha Singida United kwenye Uwanja wake wa Ushirika mkoani Kilimanjaro.
Tanzania Prisons itavaana na Kagera Sugar Uwanja wa Sokoine, Mbao FC itakuwa CCM Kirumba ikicheza na Ruvu Shooting wakati Namungo FC itakuwa Uwanja wa nyumbani wa Majaliwa ikiikaribisha Lipuli FC huku Ndanda FC nayo ikiwa nyumbani Nangwanda kucheza na Mtibwa Sugar.
Kocha wa Namungo FC, Hitimana Thiery alisema wamejiandaa vyema kuwakabili wapinzani wao, kutokana na matokeo mabaya ambayo wameyapata katika michezo iliyopita wakiwa nje ya uwanja wao.
Kocha wa Polisi Tanzania, Ali Mtuli aliwaomba mashabiki wa mkoa huo kujitokeza kwa wingi kuwapa nguvu wachezaji wao kwenye mchezo huo wa pili katika uwanja wao tangu kuanza kwa ligi msimu huu.