Mkuu wa mitandao ya kijamii wa klabu ya Napoli, Alessio Fortino ameamua kuacha kazi baada ya Victor Osimhen kudhihakiwa kutokana na video mbili zilizopostiwa na klabu hiyo katika mtandao wa TikTok.
Mshambuliaji huyo alichekwa na kusemwa vibaya kwa kukosa penati dhidi ya Bologna kabla hajaitwa ”Nazi” neno ambalo limechukuliwa kuwa ni la Kibaguzi.
Baada ya video hizo kusambaa, wakala wa Osimhen alijibu na kusema kitendo hiko hakikubaliki na alitishia kuishtaki klabu.
Baadaye klabu hiyo ilizifuta video hizo na ilijibu kwa kusema video zile hazikuwa na nia mbaya.
Kupitia mtandao wa Instagram Fortino ametangaza uamuzi huo kwa kuandika ” Leo , baada ya siku 805 safari yangu kikazi na Napoli inafikia mwisho”.
Vilevile aliwashukuru kwa kila kitu wafanyakazi wenzake wote, washirika na mashabiki.