Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF ) Wallace Karia amesema Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika (CAF) limetoa vifaa vya usaidizi wa video kwa Waamuzi yaani VAR ambayo itakuwa inatumika katika mechi za Ligi Kuu Tanzania Bara na tayari Wataalamu wameshakuja nchini kwa ajili ya kutoa mafunzo.
Karia ameyasema hayo leo kwenye Mkutano Mkuu wa TFF wa 18 uliofanyika Mkoani Iringa ambapo amesema vifaa hivyo vitafungwa katika viwanja vitakavyokidhi vigezo vya CAF na FIFA.
“ Tumepata VAR ambayo itakuwa kwenye uwanja wa Benjamin Mkapa, Wataalamu wameingia jana na watatoa mafunzo lakini kwenye viwanja ambavyo vina vigezo vyote na tutaangalia maboresho ya viwanja ili tuweze kuwa na VAR kila sehemu.”