Mchoro wa mwonekano wa uwanja mpya wa Manchester United unaotambulika kwa jina la mradi kama ‘Wembley ya Kaskazini’ umewekwa hadharani namna unavyokuwa. Mmiliki mwenza wa klabu hiyo yenye maskani yake Old Trafford, bilionea Sir Jim Ratcliffe amepanga kujenga uwanja wa kisasa utakaokuwa bora kuliko wa timu nyingine zote huko Ulaya.
Wakati uwanja wa sasa wa Old Trafford, ukiwa na uwezo wa kuingiza watazamaji 75,000, unahitajika kuboreshwa kwa kujengwa upya ambapo gharama zake zinaweza kufika Pauni 1 bilioni (Sh 3.2 trillion) Uwanja huo mpya utahusisha teknolojia zote kuanzia kwenye paa, ambapo tajiri Sir Jim amevutiwa na uwanja mpya wa Real Madrid, ule wa Tottenham Hotspur, hivyo anataka kuifanya Old Trafford kuwa matata zaidi. Na mpango ni kwamba uwanja huo uwe na uwezo wa kuingiza watazamaji 100,000.
Kwenye mpango wa ujenzi huo, bilionea huyo ametengeneza timu maalumu itakayoongozwa na Lord Sebastian Coe, ambapo Gary Neville atakuwapo pia kwenye wajumbe wa kuwezesha ujenzi wa uwanja huo.