Hadi kufika Jumatatu ya Januari 15, 2024 majibu yatakuwa yamepatikana ya mchezaji gani anaondoka kwenye timu na nani anajiunga, kwani kwa sasa viongozi wanakimbizana kuhitaji saini zao.
NEVER TIGERE
Winga Never Tigere, msimu uliopita alikuwa na Ihefu, mkataba wake ulimalizika tangu Desemba na sasa timu hiyo imempa mkataba mpya, anaouangalia kama una maslahi naye.
Winga huyo aliyewahi kuichezea Azam, FC alipopigiwa simu kufafanua juu ya jambo hilo, amesema "Nipo nchini kwetu Zimbabwe tangu Desemba baada ya kumaliza mkataba, nimetafutwa na timu mbalimbali za huku kwetu pamoja na za Tanzania ikiwemo Ihefu"
HAFIZ KONKONI
Mshambuliaji wa Yanga hadi sasa kacheza jumla ya dakika 189 dhidi ya KMC (26) na alifunga bao moja, JKT Tanzania (59), Geita Gold (31), Azam Fc (dakika moja) na Singida Fountain Gate (72), inasemekana anaweza akatua Ihefu kwa mkopo.
Jina la Konkoni linatajwa kupunguzwa, kutokana na idadi ya wachezaji wa kigeni kuzidi Yanga ili kumpisha Augustine Okrah na sasa inasemekana mazungumzo yanafanyika baina ya viongozi wa Yanga na Ihefu ila akacheze kwa mkopo.
RASHID JUMA / CHARLES ILANFYA
Winga Rashid Juma na mshambuliaji Charles Ilanfya ,wamemalizana na Mtibwa Sugar na muda wowote wataingia kambini na kila mmoja amesaini miezi sita na wamekiri hilo.
Rashid "Najiunga kambini Jumamosi, lakini sitaacha kuwashukuru wachezaji wenzake wa Ihefu, makocha pamoja na viongozi kwa ushirikiano wao mzuri."
Ilanfya"Ni kweli nimesaini miezi sita, narejea nyumbani kwenda kupambania timu isishuke daraja."
ABDALLAH HAMIS
Tangu ajiunge Simba msimu huu, akitokea timu ya Orapa United FC ya Botswana, amecheza dakika tano dhidi ya KMC na ametemwa na klabu hiyo na sasa anahusishwa na Namungo FC na Ihefu.
NASSOR KAPAMA
Kiraka huyo hakuwa na nafasi ya kucheza Simba tangu alipojiunga nayo msimu uliopita, akitokea Kagera Sugar na sasa anatajwa kuhitajika na Ihefu, Mtibwa Sugar na Geita Gold na ameishaachana na Wanamsimbazi hao.
JIMSON MWANUKE
Kuna wakati alikuwa anapata nafasi ya kucheza chini ya makocha tofauti, lakini hakuweza kuwashawishi kuwa tegemeo kwenye kikosi cha kwanza cha Simba, Mwanuke kwa sasa anatajwa kutafutwa timu mbalimbali ikiwemo JKT Tanzania, Mtibwa Sugar na Geita Gold.
Hizo ni timu baadhi tu, kwani zipo nyingi zinazotema wachezaji na wengine kusajili.