Dar es Salaam. Wakati Yanga kikiendelea kujifua Morogoro, mabeki wake Juma Abdul, Kelvin Yondani na Andrew Vicent bado hawajajiunga na kambi hiyo wakishindikiza kulipwa malimbikizo yao ya mishahara yao.
Lakini, wakati Yondani na Dante wakishindwa kujiunga na kikosi hicho, jana walikuwa kwenye kambi ya Taifa Stars, kujindaa kwa mchezo dhidi ya Harambee Stars.
Mwanaspoti lilipomuuliza Saleh kuhusu kutoonekana kwa wachezaji hao tangu kuanza kambi, alikiri hawakuwepo huku akieleza amesharipoti suala hilo kwa uongozi wa juu.
“Wachezaji hao hawajajiunga na kambi na sijajua sababu hivyo, tumetoa taarifa kwa uongozi wa juu hivyo, ni vyema mkawauliza wenyewe huko,” alisema.
Hata hivyo, jitihada za kumtafuta Mwenyekiti wa Yanga, Dk Mshindo Msolla na Makamu wake Fredrick Mwakalebela hazikuweza kuzaa matunda hata kupitia simu zao za kiganjani.
Kwa upande wake, Juma Abdul alikiri kutoingia kambini huku akieleza bado hajalipwa fedha zake za usajili na mishahara.
Pia Soma
- Serikali: Asilimia 49 za uwekezaji Simba, Yanga si wa mtu mmoja
- Bondia afariki kwa kipigo
- Alichokifanya Cardi B kwa Offset hiki hapa
Alisema mabosi wa Yanga waliahidi kutekeleza madai yake, lakini wameshindwa kutenda haki ahadi yao kwake.
“Unajua wachezaji tulikwenda pale Azam kuanzisha kubwa kuliko, tulikuwa katika wakati mgumu na ndipo tukafanya jambo lile na tuliipambania timu mpaka ligi imemalizika,” alisema.
Naye Dante alisema hayupo kambini kutokana na kutolipwa madai yake na hakuna dalili za kulipwa.
Hata hivyo, kwa upande wa Yondani hakuweza kupatikana kuzungumzia madai yake na baada ya mazoezi ya Stars alitoweka zake.
Yondani katika mtandao wake wa Istagram aliposti picha ya Tupac iliyoandikwa ‘Only God can judge me’ yenye tafsiri ‘Mungu pekee atanihukumu’ posti hiyo ilipata like 2913 na wachangiaji 105 ndani muda mfupi.
Msimu uliopita Yondani aligomea kusaini mkataba mpya na Yanga hadi pale Abass Tarimba alipojitolea kumlipa fedha za usajili huku Dante akipewa ahadi ya kulipwa.