Wachezaji wa timu ya Taifa ya Tanzania ya Wanawake (Twiga Stars) wamempongeza Rais Samiah Suluhu kwa kuonyesha nia ya kudhamini mashindano ya CECAFA kwa upande wanawake.
Mwishoni mwa wiki iliyopita wakati Rais Samia akiipongeza Timu ya Taifa vijana ya wanaume ( U 20) baada ya kutwaa ubingwa wa CECAFA , aliahidi kudhamini mashindano ya CECAFA kwa wanawake yatakayofanyika mwakani.
Pia alitoa kauli jinsi wachezaji wa kike wanavyojiweka kiume na kuwataka kubadilika kauli ambayo iliizua mjadala kwa wadau soka.
Wakizungumza leo katika mkutano wa waandishi wahabari, wachezaji wa Twiga Stars wamempongeza rais Samia kwa kuwa mstari wa mbele kukuza soka la wanawake.
Esther Mabanza ametoa shukrani kwa Rais Samia kwa kuwa bega kwa bega kila wakati na kuwataka wadhamini kujitokeza kuunga mkono juhudi za Rais kukuza soka la wanawake.
“Tunamshukuru Rais kwa kutuunga mkono kwa kudhamini soka la mwanawake na pia tunaomba wadau mbali mbali nao wajitokeze ili kupunguza changamoto zilizopo katika soka la wanawake”, amesema Mabanza.
Pia mchezaji mwengine Janeth Christopher licha ya kumpongeza Rais Samia amewaomba wadau wasiichukulie hasi kauli ya mama kwani inawapa chachu wao kama wachezaji kupambana.
“Kuna kauli alitoa Rais ambae ni kama mama yetu kuhusu sisi wachezaji wakike kujiweka kama wanaume kauli ambayo imechukuliwa tofauti na baadhi ya watu . Tunawaomba wasiichukulie vibaya kwani kauli ile mama ameitoa kama kutufunza hivyo tunaifanyia kazi na tunaendeleza mapambano,” amesema Janeth.
Naye Stumai Abdallah amesema mchezo wa soka wanaocheza unahitaji kuwa na nguvu na sio kuwa lele mama, tunafanya mazoezi ili kujiweka fitii hivyo watu wasiwachukulie kiume.
“Licha ya kauli ya mama kuchukuliwa hasi na baadhi ya wadau wa soka ,sisi kama wachezaji imezidi morali ya kupambana na watu inabidi watambue mchezo wa soka sio lele mama na mavazi tunayovaa ni ya kawaida na yanavaliwa na kila mtu katika jamii, “ amesema Stumai.