Twiga Stars ina kibarua kigumu ugenini leo wakati itakapojiuliza tena dhidi ya Namibia katika mechi ya kuwania kufuzu ushiriki wa fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika kwa timu za wanawake, huku ikiahidi itapambana itoboe.
Kipigo cha mabao 2-1 nyumbani katika mechi iliyopigwa Jumatano kwenye Uwanja wa Benjamin Mkapa kinailazimisha Twiga kushinda zaidi ya bao moja leo ili isonge mbele kuingia raundi ya pili na kuumana mshindi baina ya Zambia na Malawi. Mechi hiyo inapigwa kwenye Uwanja wa Dobsonville uliopo jijini Johannesburg kuanzia saa 10 jioni kwa muda wa Afrika Mashariki.
Historia nzuri ya matokeo mazuri kwa Twiga ikiwa Sauzi kunapopigwa mchezo huo inaiweka katika hali nzuri kisaikolojia ya kupata ushindi mnono ugenini.
Kocha wa Twiga Stars, Bakari Shime alisema licha ya mlima mrefu walionao, wana imani kubwa ya kupindua meza kibabe.