Michezo

Habari

Burudani

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Twiga Stars, Tanzanite wembe uleule 

8d7b5c1e21917fe4e359d4169c4a77e3.jpeg Kikosi cha Twiga Stars, kilichopo Afrika ya Kusini

Sat, 9 Oct 2021 Chanzo: www.habarileo.co.tz

Timu za Taifa za soka za wanawake, Twiga Stars na Tanzanite leo zitakuwa na kibarua cha kupeperusha bendera ya Taifa katika michuano ya kimataifa.

Twiga Stars itacheza na Malawi katika fainali ya michuano ya Cosafa kwenye uwanja wa NMB, Port Elizabert, Afrika Kusini na Tanzanite itaikaribisha Eritrea katika mchezo wa kufuzu Kombe la Dunia kwenye Uwanja wa Azam Complex, Chamazi, Dar es Salaam.

Twiga Stars ilifuzu fainali baada ya kuifunga Zambia kwa penalti 3-2 baada ya sare ya 1-1 na Malawi waliwafunga wenyeji Afrika Kusini ambao ndio bingwa mtetezi kwa mabao 3-2.

Afrika Kusini watacheza mchezo wa kutafuta mshindi wa tatu dhidi ya Zambia, kuanzia saa 6:00 mchana na mchezo wa fainali utachezwa saa 10:00 jioni.

Akizungumzia mchezo huo kocha wa Twiga Stars, Bakari Shime amesema anaamini ubingwa ni wao maana wachezaji wana ari na wanataka kurudi na kombe.

“Wachezaji wana ari na waliahidi kurudi na kombe hivyo wamenihakikishia ushindi na watacheza kufa kupona,” amesema Shime.

Twiga Stars imefika fainali kwa mara ya kwanza katika michuano hiyo ambayo hushiriki kama nchi mwalikwa baada ya timu za wanawake za U-20 na U-17 kutwaa kombe hilo mwaka juzi na mwaka jana.

Naye kocha wa Tanzanite Queens, Edna Lema amesema wamejiandaa na mchezo huo wa marudiano wa kufuzu Kombe la Dunia dhidi ya Eritrea na wana uhakika wa kulinda ushindi wa mabao 3-0 waliopata mjini Asmara.

“Tumefanya maandalizi ya kutosha na wachezaji wana ari na wanataka kufuzu kucheza Kombe la Dunia, Watanzania waje kwa wingi Chamazi kutushangilia,” amesema Edna.

Baada ya raundi ya pili itafuatiwa raundi ya tatu ambayo watacheza na mshindi kati ya Namibia au Burundi na mshindi wake ndio atakayefuzu Fainali za Kombe la Dunia zitakazofanyika Costa Rica mwakani.

Chanzo: www.habarileo.co.tz