Timu ya taifa ya wasichana chini ya umri wa miaka 20, Tanzanite imelazimishwa sare ya kufungana bao 1-1 na Nigeria leo katika mchezo wa kwanza wa Raundi ya Tatu kufuzu Kombe la Dunia mwakani nchini Colombia.
Katika mchezo mkali na wa kusisimua uliofanyika Uwanja wa Azam Complex, Dar es Salaam, Nigeria ilitangulia kwa bao la Chioma Oliseh kipindi cha kwanza, kabla ya Asnath Ubamba kuisawazishia Tanzanite kipindi cha pili.
Timu hizo zitarudiana Novemba 19 Uwanja wa Taifa wa Moshood Abiola National Stadium, Abuja na mshindi wa jumla atakutana na mshindi wa jumla kati ya DRC na Burundi katika Raundi ya Nne na ya mwisho ya mchujo wa kuwania tiketi ya Colombia 2024.
Ikumbukwe sehemu kubwa ya wachezaji wa Tanzanite ndio waliowezesha Tanzania kufuzu Fainali za Kombe la Dunia za U17 mwaka jana nchini India.