TIMU ya soka yaTanzania Prisons, imeanza kutamba ikisema inakusudia kumaliza katika nafasi nne za juu katika msimamo wa Ligi Kuu Tanzania Bara.
Prisons, imekuwa na muendelezo mzuri wa matokeo katika michezo miwili mfululizo na kukusanya pointi nne baada ya kuibana mbavu Simba na kuilazimisha sare ya bao 1-1 na baadaye kuibuka na ushindi wa bao 1-0 dhidi ya JKT Tanzania.
Kocha msaidizi wa kikosi hicho Shaaban Kazumba, alisema jana kuwa yeye pamoja na benchi lake la ufundi lengo lao ni kukusanya pointi katika kila mchezo ili kujiweka katika mazingira mazuri ya kutimiza mipango yao.
“Lengo letu sio kupata matokeo dhidi ya timu kubwa tu bali tumedhamiria kumaliza ligi katika nafasi nne za juu ikiwezekana tupate nafasi ya kuiwakilisha nchi katika michuano ya Kombe la Shirikisho mwakani,” alisema Kazumba.
Kazumba ana kaimu nafasi ya kocha mkuu, Salum Mayanga, ambaye yuko nje ya majukumu kutokana na kusumbuliwa na maradhi.
Prisons, ipo nafasi ya nane katika msimamo wa Ligi Kuu ikiwa imecheza michezo 23 na kujikusanyia pointi 31ikiwa nyuma kwa pointi nane kwa Biashara United inayoshika nafasi ya nne.