Ushindi wa mabao 7-0 dhidi ya Djibouti, umeifanya timu ya taifa soka ya wanawake ya Umri chini ya Miaka 20, kufuzu raundi ya tatu ya michuano ya kuwania fainali za Kombe la Dunia zitakazofanyika mwakani na sasa itavaana na Nigeria kwenye hatua hiyo, mechi zitakazopigwa mwezi ujao.
Tanzania imetinga hatua hiyo kwa ushindi wa jumla ya mabao 12-0 kwani kwenye mechi ya mkondo wa kwanza iliyopigwa wikiendi, ilishinda kwa mabao 5-0 na juzi jioni itadoa dozi nyingine ya 7-0 kwa mabao ya Jamila Rajabu na Winfrida Gerald kila mmoja alifunga mawili, Diana Mnally, Zainab Ally na Yasinta Joseph waliofunga bao moja kila mmoja.
Matokeo hayo yameifanya Tanzania kukutana na Nigeria katika mechi za raundi ya tatu baada ya wababe hao wa Afrika Magharibi, kupenya kiulaini kutokana na Mauritius waliokuwa wacheze nao raundi ya pili kujitoa ghafla.
Tanzania itaanzia mechi za raundi hiyo nyumbani kati ya Novemba 10-12 jijini Dar es Salaam kisha kusafiri hadi ugenini wiki moja baadaye na mshindi wa jumla atafuzu raundi ya nne kuvaana mshindi kati ya Burundi na mshindi wa mechi ya Zambia na CR Congo zilizokuwa zikirudiana jana.
Raundi hiyo ya nne ndiyo itakayokuwa ya mwisho ya kutoa washindi wanne wa kuiwakilisha Afrika katika fainali hizo zitakazofanyikia Colombia. Fainali zilizopita Afrika ziliwakilishwa na Nigeria na Ghana.