Jumapili, wiki hii timu ya taifa ‘Taifa Stars’ itakuwa kibaruani tena kukipiga dhidi ya Niger katika mchezo wa kundi F wa kuwania kufuzu fainali za mashindano ya Mataifa ya Afrika (Afcon) zitakazofanyika mwakani nchini Ivory Coast.
Katika msimamo wa kundi lenye timu nne, Stars inashika nafasi ya pili ikiwa na pointi nne sawa na Uganda ya tatu zikiongozwa na Algeria yenye alama 12 na ambayo tayari imeshafuzu, hivyo Tanzania itapaswa kuifumua Niger inayoshika mkia na alama mbili ili kujiweka katika nafasi nzuri ya kufuzu.
Uganda, mshindani wa karibu wa Stars itaikaribisha Algeria katika mchezo ambao hautachezewa nchini Uganda kutokana uwanja wake mkubwa kuwa katika matengenezo ambayo yalitarajiwa kuwa yangekuwa yamekamilika, lakini hadi wiki za karibuni hali ilikuwa bado.
Hata hivyo, vyovyote ilivyo kikosi cha Stars chini ya kocha Adel Amrouche kitapaswa kujipanga vilivyo dhidi ya Niger ambayo licha ya kuwa na matokeo mabovu, lakini inaundwa na nyota wengi wanaokipiga katika mataifa ya Ulaya, hivyo wana uwezo wa kuamua mchezo wakiamua.