Michezo

Habari

Burudani

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

TFF watafutana

60f6083de33632c0380ff909fc6271a4.jpeg TFF watafutana

Mon, 10 May 2021 Chanzo: www.habarileo.co.tz

SHIRIKISHO la Soka Tanzania (TFF) limeiagiza Bodi ya Ligi Kuu (TPLB) kutoa taarifa ya kina kuhusu kuahirishwa mechi ya Simba na Yanga juzi.

Mechi hiyo ya Ligi Kuu Tanzania Bara ilipangwa kuchezwa kwenye Uwanja wa Benjamin Mkapa saa 11 jioni, lakini saa chache kabla ya mchezo huo, TFF ilitoa taarifa ya kuisogeza mbele mpaka saa 1:00 usiku baada ya kupokea maelekezo kutoka Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo.

Taarifa hiyo ilipingwa vikali na Yanga ikitaka kanuni ifuatwe na kusisitiza kupeleka timu uwanjani katika muda uliopangwa awali, ambapo timu hiyo ilifika uwanjani katika muda huo na baadae timu hiyo iliondoka uwanjani baada ya kusubiri kwa dakika 15 wapinzani wao Simba ambao walijiandaa kucheza saa 1:00 kama ilivyoelekezwa na TFF na kupekelekea mchezo huo kutangazwa kufutwa.

Taarifa ya TFF iliyotolewa jana, pia iliitaka TPLB kushughulikia hatima ya mashabiki waliolipa viingilio kushuhudia mechi hiyo.

“TFF inapenda kuomba radhi kwa wadau wote waliolipa viingilio kuingia uwanjani, waliokuwa wakisubiri kuangalia kwenye televisheni, kusikiliza redioni na watoa huduma mbalimbali,” ilisema taarifa hiyo ya TFF iliyosainiwa na Ofisa Habari wake, Cliford Ndimbo.

“Tunaomba wapenzi wa mpira wa miguu kuwa watulivu wakati jambo hili linashughulikiwa kwa haraka kwa taratibu za kikanuni, lakini huku tukishirikiana kwa karibu na wadau wote ikiwemo serikali,” ilisema taarifa hiyo.

Aidha, taarifa hiyo ilisema, TFF imekuwa ikishirikiana na serikali kama mdau wake mkuu na itaendelea kushirikiana nayo kuhakikisha mechi zote za mpira wa miguu zinafanyika kwa amani na usalama.

“Pamoja na jambo hili kuendelea kushughulikiwa kikanuni kama tulivyoielekeza Bodi ya Ligi, TFF inaendelea kufanya vikao mbalimbali na vyombo vya serikali kuhusu tukio hilo, pia itakutana haraka na klabu hizo (Simba na Yanga),” ilisema taarifa hiyo.

Chanzo: www.habarileo.co.tz